Trusted since 2008
Study resources on Kenyaplex

Get ready-made curriculum aligned revision materials

Exam papers, notes, holiday assignments and topical questions – all aligned to the Kenyan curriculum.

Umaskini ni tatizo sugu katika jamii. Binadamu wengi hujikuta katika hali hii kwa sababu hawakubahatika kusoma. Baadhi yao huenda...

Soma taarifa hii kisha ujibu maswali

Umaskini ni tatizo sugu katika jamii. Binadamu wengi hujikuta katika hali hii kwa sababu hawakubahatika kusoma. Baadhi yao huenda walijaribu kusoma wakashindwa mapema kujipandisha kielimu. Ukosaji wa elimu huchangia sana katika kukuza ukata. Elimu huweza mtu kupata tonge kwa kujipatia kazi za kumwezesha kuyakidhi mahitaji ya maisha. Hali kadhalika, elimu humsaidia binadamu kupata maarifa mengi ya kutendea shughuli zake za kimaendeleo. Kwa mfano, kama ni wakulima wanaweza kutumia pembejeo zifaazo ili kuboresha uzalishaji wa mazao. Wakulima wenye elimu hawatapendelea njia duni za kuendeleza kilimo kama vile kutumia visagilima na mbinu nyingine za kijadi. Badala yake watatumia njia za kisasa za kuvunia mazao yao.
Umaskini mwingine huwa mwiba wa kujichoma. Baadhi ya watu ni mikunguni. Kulaza damu kwao kunawafanya kuwa wategemezi katika familia na jamii kwa jumla. Kwa vile hawajazoea kuinamia cha mvunguni, hata wakifunzwa kuchakura hawawezi. Ili kujaribu kuutibu uwele wao na ufukara baadhi yao hutafuta njia za mkato kama vile upwekuzi wa vitu vya wale waliojitahidi. Wakifanikiwa huweza kufurisha vibindo vyao. Hata hivyo mkono mrefu wa walinda usalama ukiwakumbatia wao hubakia kusagika kwa dhiki isiyomithilika ndani ya magereza.
Majanga ya kimaumbile kama vile mitetemeko ya ardhi, mikurupuko ya maradhi hatari, moto, ukame na mafuriko huchangia na kuzidisha umaskini. Matukio hayo yakiandama kidindia watu wengi huhasirika. Licha ya mali nyingi kupotea, manusura huachwa wakiwa maskini hohehahe. Matumizi yao hupotea kwani wengi huhitajika kuanza maisha upya.
Vijana ni nguzo muhimu katika maendeleo ya nchi yoyote ile. Endapo watajiingiza katika uraibu wa dawa za kulevya, wataathirika wao wenyewe na jamii kwa jumla. Pamoja na kuwa vijana hawa hufuja pesa nyingi katika ununuzi wa dawa hizi, dawa zenyewe huwadhoofisha na kuwapoka nguvu za kushiriki katika uzalishaji mali. Kutokana na hali hii,umaskini hupaliliwa na kushamiri zaidi.
Umaskini huzua matatizo mbalimbali katika jamii. Ufukara huchachawiza juhudi za serikali za kuwapa raia wake mahitaji ya kimsingi kama vile huduma za afya. Pia umaskini husababisha maovu mbalimbali ya kijamii kama vile mauaji na ukahaba.
Baadhi ya wanajamii huona kwamba njia ya kipekee ya kukabiliana na changamoto zinazosababishwa na hali ya ulitima ni kupitia kwa biashara haramu. Hali hii huchochea zaidi kudorora kwa maadili ya kijamii.
Mataifa mbalimbali ulimwenguni yamezua mikakati mahsusi ya kukabiliana na umaskini. Baadhi ya mataifa yamebuni utaratibu maalum wa kupunguza mwanya mkubwa uliopo kati ya matajiri na maskini. Mojawapo ya mipango hiyo ni kupandisha viwango vya kodi inayotozwa wenye mishahara minono na wafanyibiashara wenye pato kubwa. Aidha huduma za burudani hutozwa kodi ya kiwango cha juu. Kupitia kwa kodi hizo, na njia nyinginezo, serikali za nchi hizo hupata pesa za kuwahudumia maskini.
Mataifa yanayoendelea yanaweza kuwakwamua wananchi kiuchumi kwa kuwapa wahitaji mitaji ya kuanzisha miradi mbalimbali ya kimaendeleo. Mifano ya miradi hiyo ni viwanda vya ‘Jua kali’, ususi wa vikapu na uchongaji wa vinyago. Hali kadhalika, serikali inaweza kuwatafutia masoko ya nje wafanyi biashara wadogo wadogo. Aidha, serikali inaweza kupunguza ushuru kwa bidhaa zinazoagizwa na masoko ya nje wafanyibiashara wa aina hiyo. Mathalan, ushuru unaotozwa nguo kuukuu zinazoingizwa nchini ukipunguzwa, wauzaji wa nguo hizi watafaidika zaidi na hali ya umaskini itaendelea kupungua.
Sehemu za mashambani ni mhimili mkubwa wa uchumi. Ingawa kumekuwa na juhudi za kuzistawisha sehemu hizi kwa kusambaza huduma za umeme na maji kwa gharama nafuu, bado hali haijawa ya kuridhirisha. Ili kuimarisha sehemu hizi na kukabiliana vilivyo na tatizo la umaskini, hatuna budi kusambaza huduma hizi hasa katika sehemu kame. Sehemu hizi zikipata maji, kilimo chenye natija kitaendelezwa na umaskini utakuwa karibu kuzikwa katika kaburi la sahau. Ikiwa tutazitekeleza sehemu hizi, vijana wanaoweza kusistawisha watahamia mjini kutafuta maisha ‘bora’. Hali hii itazidisha msongomano wa watu mjini.
Umaskini ni nduli ambaye lazima aangamizwe ima fa ima. Vijana hawana budi kubadili mtazamo wao hasa kuhusu kazi za mashambani na kujitahidi kuimarisha kilimo. Fauka ya hayo, mifumo mwafaka ya elimu ibuniwe ili kukidhi mahitaji ya kiuchumi ya taifa. Badala ya kuhimiza elimu ya kinadharia, elimu tekelezi isisitizwe zaidi ili wale wanaokosa kazi za kiafisi waweze kujiajiri katika kazi za kiufundi. Ukusanyaji wa ushuru uimarishwe zaidi. Hali ya usalama iendelee kustawishwa ili kuzidi kuwavutia wawekezaji, na hivyo kubuni nafasi zaidi za kazi.


(a)Kulingana na kifungu ‘umasikini ni hali inayoletwa na udhaifu wa mtu binafsi’. Jadili
(maneno 30-40)
(b)Jamii ina uwezo wa kukabiliana na hali ya umaskini inayowakumba raia wake. Thibitisha
kwa mujibu wa kifungu (maneno 40-50)

Answers


Maurice
(a) i. Ukosefu wa elimu
ii. Kulaza damu/ uzembe
iii. Ufuaji
iv. Umaskini pia huletwa na majanga ya kimaumbile Kama vile:-
- Mitetemeko ya ardhi
- Maradhi hatari
- Moto
- Ukame
- Mafuriko


(b) - Kupunguza mwanya mkubwa uliopo kati ya matajiri na maskini
- Kupandisha viwango vya kodi inayotozwa wenye mshahara mnono na wafanya biashara wenye pato kubwa
- Huduma za burudani kutozwa kodi ya kiwango cha juu
- Elimu tekelezi isisitizwe
- Kupunguza ushuru kwa bidhaa zinazoagizwa
- Kuwapa wahitaji mitaji ya kuanzisha miradi mbalimbali ya kimaendeleo
- Kusambaza huduma za umeme na maji sehemu za mashambani
maurice.mutuku answered the question on October 4, 2019 at 10:09

Answer Attachments

Exams With Marking Schemes

Related Questions

  • Andika wingi wa sentensi zifuatazo; i) Sokwe aliukwea mti huo kwa kasi.ii) Mshale mkali ulitumiwa kumwua samba. (Solved)

    Andika wingi wa sentensi zifuatazo;
    i) Sokwe aliukwea mti huo kwa kasi.
    ii) Mshale mkali ulitumiwa kumwua samba.

    Date posted: October 4, 2019 .    Answers (1)

  • Tumia neno "vile" kama. i) Kivumishi … ii) Kiwakilishi iii) Kielezi (Solved)

    Tumia neno "vile" kama.
    i) Kivumishi …
    ii) Kiwakilishi
    iii) Kielezi

    Date posted: October 4, 2019 .    Answers (1)

  • Eleza maana mbili za sentensi ifuatayo (Solved)

    Eleza maana mbili za sentensi ifuatayo.
    Nitakuja kukagua kazi hiyo baada ya saa mbili.

    Date posted: October 4, 2019 .    Answers (1)

  • Waajiri wengi wanazilaumu taasisi za elimu kwa kukosa kutoa wafanya kazi wenye ujuzi tosha, hasa wa kiteknolojia za kisasa kama kutumia... (Solved)

    Soma makala yafuatayo kisha kisha ujibu maswali:-

    Waajiri wengi wanazilaumu taasisi za elimu kwa kukosa kutoa wafanya kazi wenye ujuzi tosha, hasa wa kiteknolojia za kisasa kama kutumia kompyuta kutenda kazi mbalimbali. Hali hii imekuwa ya kuhuzunisha sana.
    Ujuzi wa kuweza kutumia Kompyuta unaweza kumfaa mwanafunzi hata anapokosa nafasi ya kujiunga na chuo kikuu kwa vile anaweza kuendelea na elimu yake kupitia kwa elimu mtandao. Pia anaweza kufanya utafiti wa kina kupitia intaneti na kwa njia hii akaimarisha elimu yake.
    Mojawapo ya njia ya kuimarisha elimu kuhusu maswala ya teknolojia ni kuanzishwa kwa mikakati mipya ya kufunza. Somo la Kompyuta laweza kuimarika mashuleni endapo kwanza walimu watahamasishwa juu ya faida za ujuzi huu.
    Kwa kutumia Kompyuta kufunza, walimu wanaweza kufunza madarasa kadhaa katika kipindi kimoja bila kulazimika kuyahudhuria. Hii itapunguza kiwango cha kazi kwa walimu kwa vile watapata muda wa kufanya utafiti mpana. Aidha, watapata habari na ufahamu zaidi wa mambo kwa kutumia mitambo ya Kompyuta kutoka kwenye intaneti, kupitia tovuti.

    Hata hivyo mipango hii inakabiliwa na changamoto kama vile bei za juu za mitambo na vifaa vya Kompyuta, ukosefu wa miundo msingi itakayowezesha utumiaji wa mitambo hii na ukosefu wa walimu waliohitimu somo la Kompyuta.
    Pia, kuna tatizo la ukosefu wa nguvu za umeme hasa maeneo ya mashambani; vile vile, katika maeneo yaya haya, wanafunzi na wazazi wengi huvichukulia somo la Kompyuta kuwa gumu na linalofaa wakaazi na wanafunzi kutoka maeneo ya mijini na linalofaa wakaazi muhimu kwao mashambani.



    Maswali
    (a) Ipe taarifa uliyoisoma anwani inayoifaa
    (b) “Hali hii imekuwa ya kuhuzunisha.” Ni hali gani inayozungumziwa katika aya ya 1?
    (c) Ujuzi wa kutumia Kompyuta unaweza kumfaidi vipi mwanafunzi?
    (d) Mikakati mipya ya kuimarisha elimu kuhusu maswala ya teknolojia inakabiliwa na
    vizingiti vipi?
    (e) Taja manufaa mawili ambayo mwalimu anaweza kupata kutokana na ujuzi wa teknolojia
    ya Kompyuta
    (f) Andika msamiati mwafaka zaidi kwa maneno yafuatayo:
    (i) Kompyuta
    (ii) Intaneti

    Date posted: October 4, 2019 .    Answers (1)

  • Licha ya kuwa na historia ya kiasi, maisha ya binadamu ni kioja kikubwa. Hebu jiulize jinsi uhai wako wewe mwenyewe ulivyoanza sembuse... (Solved)

    Soma taarifa hii kisha ujibu maswali

    Licha ya kuwa na historia ya kiasi, maisha ya binadamu ni kioja kikubwa. Hebu jiulize jinsi uhai wako wewe mwenyewe ulivyoanza sembuse unavyoweza kupumua na kuishi siku nenda siku rudi.
    Dini zimefahamisha kuwa sisi binadamu tumeumbwa na Mwenyezi Muumba. Hata hivyo muumba hutumia mume na mke kutuanzishia maisha yetu humu humu duniani. Uhai wa hapa duniani huanzia katika tumbo la mwanamke muda mfupi tu baada ya mume na mke kushirikiana katika tendo la kujamiana. Katika ngono hii yenye ufanisi, mbegu moja ya manii kutoka kwa mwanamume, hudunga na kujiingiza katika yai la mwanamke huku ikilirutubisha. Tangu hapo mtu huwa na mama akawa mjamzito. Hatua ya kwanza ya uhai!
    Wanasayansi wametuthibitishia kuwa mbegu katika shahawa kutoka kwa mwanamume ina kromosomu ishirini na tatu (23) nalo yai la mwanamke lina idadi iyo hiyo ya kromosomu. Basi katika hatua ya kwanza ya uhai wake, binadamu ana kromosomu arubaini na sita (46).
    Kromosomu hizo zote ndizo humfanya mtu kuwa mkamilifu kwa kukadiria mambo mbalimbali adhimu. Kwa mfano, kukadiria kama kiumbe kitakuwa cha kike au cha kiume, mtu mweupe au mtu mweusi, mwerevu au wa wakia chache, mwenye nywele za singa au za kipilipili, atakuwa na damu ya namna gani, michoro ya vidole vyake itakuwa vipi na hata utu wake utakuwa wa namna gani katika siku za usoni.
    Elimu yote anayopata mtu kutoka kwa jamii na mazingira huweza tu kujenga juu ya yaliyokwisha kuanzilishwa na kromosomu katika yai lililorutubishwa tumboni.
    Haihalisi kabisa kufikiria kwamba huwa katika hali ya ukupe. La hasha! Yeye hujitegemea kwa vyovyote na ana upekee wake. Hatangamani na mama yake. Roho yake humdunda mwenyewe na damu yake ambayo huenda ikawa tofauti kabisa na ya mama yake, humtembea na kumpiga mishipani mwake. Isitoshe, yeye si mojawapo katika viungo vya mwili wa mama yake vinavyomdhibiti katika himaya yake ndogo.
    Amini usiamini, hapana binadamu hata mmoja ambaye amewahi kuwa sawa kimaumbile na mwingine na wala hatakuweko. Hata watoto pacha kutoka yai moja la mama hawawi sawa, lazima watofautiane. Si nadra kusikia mtu amepata ajali akahitaji msaada wa damu, na pakakosekana kabisa mtu hata mmoja kutoka jamaa yake wa kimwauni. Basi ukistaajabu ya Musa utaona ya Firauni.

    1. Ipe taarifa uliosoma anwani mwafaka
    2. Mwandishi ana maana gani anaposema ‘ngono yenye ufanisi’?
    3. Uchunguzi wa sayansi umekita mizizi imani gani ya kidini?
    4. Taja majukumu yoyote matano yanayotekelezwa na kromosomu
    5. Katika makala, elimu kutoka kwa jamii na mazingira yaelekea kuwa bure ghali. Kwa nini?
    6. Eleza maana ya maneno yafuatayo kama yalivyotumika katika makala:-
    (i) huwa katika hali ya ukupe…
    (ii) himaya
    (iii) hatangamani na mama yake

    Date posted: October 4, 2019 .    Answers (1)

  • Eleza sifa tano za sajili ya magazeti. (Solved)

    Eleza sifa tano za sajili ya magazeti.

    Date posted: October 4, 2019 .    Answers (1)

  • Andika kinyume. Ukipitia kwao utalaaniwa. (Solved)

    Andika kinyume.
    Ukipitia kwao utalaaniwa.

    Date posted: October 4, 2019 .    Answers (1)

  • Andika maana mbili za neno "mlango". (Solved)

    Andika maana mbili za neno "mlango".

    Date posted: October 4, 2019 .    Answers (1)

  • Jibu kulingana na maagizo. (i) Ufisadi (unda kitenzi) (ii) - pya (unda nomino) (Solved)

    Jibu kulingana na maagizo.
    (i) Ufisadi (unda kitenzi)
    (ii) - pya (unda nomino)

    Date posted: October 4, 2019 .    Answers (1)

  • Kanusha sentensi hii katika hali ya "a" Kibofu hupaa angani. (Solved)

    Kanusha sentensi hii katika hali ya "a"
    Kibofu hupaa angani.

    Date posted: October 4, 2019 .    Answers (1)

  • CHIMBUKO LA USHAIRI Ushairi ni fani kongwe kama mwanadamu mwenyewe alivyo mkongwe duniani. Na mashairi yamekuwepo kitambo sana hata kabla ya lugha... (Solved)

    CHIMBUKO LA USHAIRI
    Ushairi ni fani kongwe kama mwanadamu mwenyewe alivyo mkongwe duniani. Na mashairi yamekuwepo kitambo sana hata kabla ya lugha ya Kiswahili bado haijanawiri na kushamiri kama ilivyo hivi leo. Ndipo tunasikia kuna mashiri ya kipemba, mashairi ya kimvita, mashairi ya kivumba, mashairi ya kipate, mashairi ya kiyunani, ya kirumi na kadhalika,. Almradi kila jamii na kila kabila lilikuwa na mashairi yake.
    Katika utafiti na kongomano zao, wataalam wa arudhi za Kiswahili asili wamechambua na kufafanua kwamba mashairi ya Kiswahili asili yake ni nyimbo za jadi zilizokuwa zikiimbwa na manju, wangoi au waimbaji stadi wa tangu na tangu walipojumuika katika matukio na hafla mbalimbali kama za jando, arusi, matanga, ngoma na shangwe zao za maishani.
    Nyimbo hizi zilitumiwa na watangulizi wetu, kidhamira hazikuhitalafiana hata kidogo na mashairi ya Kiswahili tunayohimiza wakati huu. Farka iko katika lugha na umbo kwani kila jamii ilitumia lugha yake na lahaja ya mazingira yake. Na kwa upande wa umbo, tungo hizo za awali kabisa hazikuwa na sanaa kwa maana ya ushauri tunauona leo. Bali tungo hizo zilijengeka katika nguzo mbili kuu. Kwanza ni uzito wa mawazo maadilifu ambayo yalitaamaniwa sana. Na pili ni mizani ya sauti ya manju kulingana na lahani, pumzi zake pamoja na madoido katika uimbaji ambao ulikuwa burudani naathari katika noyo za wasikilizaji wake.
    Kwa kifupi ni kwamba, nyimbo hizo ziliuhifaid umma kwa njia mbili, mawaidha kwa mapana na taathira au jadhba kutokana na sauti tamu ya manju.
    Kama utakubalika, basi huo ndio ushairi wa awali kabisa ullioambatana na nyimbo zetu za kienyeji. Kila kabila katika nchi zetu lilikuwa na ushauri wake au nyimbo zake zenye undani uliolenga sababu maalum na tukio maalum katika jamii.
    Nyimbo kama hizo kwa jina la sasa tunaweza kuita mashairi ndizo zile zilizoitwa ‘mwali’ na wakamba; gichandi kwa ‘wakikuyu’; ‘gigia gi sigele’ kwa waluo na ‘wagashe’ kwa wasukuma zilikuwa na undani wa kipekee tena uliodidimia ambao si bure kutolewa hadharani.
    Aina za mashairi ya watu wa mwambao ni kama lelemama, misemele, gungu, nyiso, kongozi n.k.
    (Walla Bin Walla – Malenga wa Ziwa Kuu , E.A.E.P)



    1. Ni nini haswa chimbuko la ushairi?
    2. Kulingana na kifungu hiki, ni nini umuhimu wa ushairi ?
    3. Ni maswala gani yaliyowapendeza wasikilizaji wa tungo hizo za zama ?
    4. Tofauti kati ya nyimbo za zama na ushairi wa leo upo kwenye vipengele gani viwili ?
    5. Kifungu : ‘haijanawiri na kushamiri’ ina maana gani katika lugha nyepesi ?
    6. Eleza maana ya :
    (a) Kongamano …
    (b) Jadhiba
    (c) Farka
    (d) Awali..

    Date posted: October 4, 2019 .    Answers (1)

  • Andika katika msemo halisi. Mwalimu alishangaa ni kwa nini Juma hakuwa amebeba mkoba wake siku hiyo. (Solved)

    Andika katika msemo halisi.
    Mwalimu alishangaa ni kwa nini Juma hakuwa amebeba mkoba wake siku hiyo.

    Date posted: October 4, 2019 .    Answers (1)

  • Andika sentensi ifuatayo kwa udogo wingi. Mtu yule haachi kuandamana na mbwa wake aliyedhoofika kiafya. (Solved)

    Andika sentensi ifuatayo kwa udogo wingi.
    Mtu yule haachi kuandamana na mbwa wake aliyedhoofika kiafya.

    Date posted: October 4, 2019 .    Answers (1)

  • Tunga sentensi moja yenye kishazi huru na kishazi kitegemezi ukitumia "O" rejeshi tamati. (Solved)

    Tunga sentensi moja yenye kishazi huru na kishazi kitegemezi ukitumia "O" rejeshi tamati.

    Date posted: October 4, 2019 .    Answers (1)

  • Changanua sentensi hii kwa kutumia jedwali. Mama alilima kwa bidii ingawa hakupata faida. (Solved)

    Changanua sentensi hii kwa kutumia jedwali.
    Mama alilima kwa bidii ingawa hakupata faida.

    Date posted: October 4, 2019 .    Answers (1)

  • Tunga sentensi ukitumia kitenzi cha katika hali ya kutendwa. (Solved)

    Tunga sentensi ukitumia kitenzi cha katika hali ya kutendwa.

    Date posted: October 4, 2019 .    Answers (1)

  • Bainisha shamirisho na chagizo katika sentensi ifuatayo. Kimathi alimwandikia babake barua kwa kalamu jana jioni. (Solved)

    Bainisha shamirisho na chagizo katika sentensi ifuatayo.
    Kimathi alimwandikia babake barua kwa kalamu jana jioni.

    Date posted: October 4, 2019 .    Answers (1)

  • Asifuye mvua imemnyea. Huu ni msemo wenye hakika isiopingika, na kutilia shaka ni sawa na kudai jua linaweza kubadilika na kuchomozea upande... (Solved)

    Soma taarifa hii kisha ujibu maswali

    Asifuye mvua imemnyea. Huu ni msemo wenye hakika isiopingika, na kutilia shaka ni sawa na kudai jua linaweza kubadilika na kuchomozea upande wa magharibi badala ya mashariki. Huu ndio ukweli uliodhihirika juzi katika vyombo vyetu vya magazeti.
    Lisemwalo lipo, na kama halipo li njiani. Waama, pafukapo moshi pana moto. Mwanafunzi mmoja wa kike kwa jina P.N. katika chuo kikuu kimojawapo nchini alishangaza umma wa Kenya na ulimwengu kwa jumla alipodai kuwaambukiza wanafunzi wenzake wa kiume mia moja na ishirini na wanne virusi vya Ukimwi.
    Kisa na maana? Aliambukizwa Ukimwi na mwanafunzi mwenzake aliyekuwa akifanya majaribio ya ualimu katika shule yao ya upili. Baada ya kushawishika sana alijuana naye kimwili, na matokeo yakawa kifo ambacho sasa alikuwa anawagawia wenzake.
    Kisa kama hiki kinachangia kueleza kina kirefu cha kutamauka na upweke ambao maisha ya waja wengi yameingia kiasi cha kuwaacha wanyama ijapo wanaenda kwa miguu miwili bado. Katika mojawapo ya mafunzo ya kidini ambayo Padre alinifunza mimi na wanafunzi wenzangu, tuliambiwa kisasi ni chake Mola, sisi waja wetu ni kushukuru tu. Mbona basi mwanafunzi kama huyu kutaka kulipiza?
    Ima fa ima, na waswahili husema, “mlaumu nunda na kuku pia”. Huyu mwanafunzi hawezi kuachiwa atende alivyotenda. Aliyekula naye raha alikuwa mtu aliyefahamika vizuri sana kwake. Isitoshe, huenda wakati huo alikosana na mama na baba kulala nje. Huenda alikosana na ndugu zake kwa kuepa nyumbani usiku wa manane kwenda kumwona huyu kalameni. Huenda alikosana na mwalimu wake kwa sababu kiburi kilianza kuingia. Kwa vyovyote vile, alikula raha na hastahili kuwaadhibu watu wasio na hatia kufidia makosa yake. Je, kama yeye na huyo jamaa wasingekuwa na Ukimwi, raha kiasi gani wangezila hadi leo?
    Jamii na watu wote kwa jumla hawana budi basi kulaani vitendo vya P.N. vya kuambukiza wanafunzi wenzake virusi huku akijua. Hili ni kosa ambalo linastahili adhabu ya kifo. Dawa ya moto ni moto ni adhabu inastahili kuchukuliwa haraka ili P.N. ambaye tayari amekiri hatia, atiwe nguvuni na adhabu itolewe.
    Barua ya P.N. inafafanua jambo jingine sugu. Kwamba kiwango cha maadili katika vyuo vyetu kimezorota kiasi cha kufanyiana unyama usiosemeka. Vijana wengi siku hizi wanashiriki tendo la ndoa bila haya. Huu upotofu wa maadili katika jamii wapaswa kushutumiwa na wote. P.N. hana sababu yoyote ya kibinadamu, kidini au kitu chochote kile kudai haki kwa uovu huo wake.


    1.Taja kichwa kwa makala haya
    2. Katika aya mbili za kwanza, mwandishi anamlaumu mwanafunzi kwa kosa gani? Eleza chanzo cha tabia za P.N
    4. Mwandishi wa taarifa hii anataka P.N achukuliwe hatua gani? Kwa nini?
    5. Barua ya P.N. bila shaka imeonyesha uvumbuzi mpya. Utaje
    6. Eleza maana ya vifungu hivi kama vilivyotumiwa katika taarifa:
    (a) Kina kirefu cha kutamauka
    (b) Ima fa ima
    (c) Kufidia makosa yake

    Date posted: October 4, 2019 .    Answers (1)

  • Tunga sentensi kwa kutumia. (i) Kivumishi cha "ki" ya mfanano. (ii) Kielezi cha kiasi cha jumla. (Solved)

    Tunga sentensi kwa kutumia.
    (i) Kivumishi cha "ki" ya mfanano.
    (ii) Kielezi cha kiasi cha jumla.

    Date posted: October 4, 2019 .    Answers (1)

  • Uundaji wa istilahi – hasa za lugha ya Kiswahili ni shughuli nyeti na nzito hivi kwamba, haipaswi kupapiwa na mtu yeyote. Hii... (Solved)

    Soma kifungu kifuatacho kisha ujibu maswali:-

    Uundaji wa istilahi – hasa za lugha ya Kiswahili ni shughuli nyeti na nzito hivi
    kwamba, haipaswi kupapiwa na mtu yeyote. Hii ni shughuli inayohitaji umakinifu zaidi kwa wanaoshiriki katika mchakato wa uundaji istilahi za kutufaa katika mawasiliano na kukuza Kiswahili kwa jumla. Ufanisi wa watu binafsi, vyombo vya habari kama vile Shirika la Habari la Kenya (KBC), Taifa Leo na mashirika mengineyo katika ukuzaji wa lugha hutegemea mno sera na utayarishaji wa serikali katika kugharamia shughuli hii. Aidha, shughuli za kukuza lugha hukwama kwa sababu ya ukosefu wa fedha pamoja na sera maalum ya serikali kuhusu lugha.
    Hata hivyo, katika kuyakwepa matatizo haya, pamekuwepo na hatua za kimataifa za kujaribu kusawazisha shughuli ya uundaji wa maneno. Hatua hii ilichochea kubuniwa kwa shirikisho la kimataifa la vyama vya usanifishaji istilahi mnamo 1936. Lengo la kitengo hiki lilikuwa ni kufafanua msingi madhubuti ya uundaji wa istilahi duniani. Kwa hakika, shirikisho hilo limesaidia mno katika kuweka misingi ya shughuli za ukuzaji wa istilahi. Misingi hiyo ni ya jumla na haihusu taaluma yoyote mahususi. Katika makala hii, tunapiga darubini baadhi ya misingi hiyo pamoja na mapendekezo yake.
    Mosi, uundaji istilahi unafaa uanzie kwenye dhana na wala sio neno. Hii ina maana kwamba, kwanza pawepo na dhana au hali ambayo inahitaji itafutiwe neno au istilahi ya kuielezea. Inasikitisha sana kwamba pana wataalamu ambao wanaukaidi au kuukiuka msingi huu. Wanataaluma hawa hufanya mambo kinyume kwa kujibunia maneno yao na kuyahifadhi kwenye mikoba yao – halafu wakasubiri dhana izuke ndiposa waipachike istilahi yao. Pili, dhana zinabuniwa au kutolea istilahi au maneo ni muhimu zielezwe kwa ukamilifu na uwazi. Istilahi zinazoundwa zinafaa ziwe fupi iwezekanavyo na ziwe na uwezo wa kuelezea dhana kwa njia inayoeleweka bila utata. Tatu, maneno yanayoundwa sharti yawe na uhusiano wa aina fulani na dhana zinazowakilishwa na maneno hayo.
    Uhusiano huo unaweza kuwa ama ni wa kimaumbile au wa kiutendaji. kwa mfano, Mzee Sheikh Nanhany wa Mombasa alipobuni istilahi ‘uka’ kwa maana ya ‘ray’. Neno hili latokana na kupambauka au (kupambazuka kwa lafudhi ya kiamu. Neno ‘image’ ni jazanda kwa Kiswahili. ‘Mirage’ kwa Kiswahili ni ‘mangati’ (kutoka kwa mang’aanti) – yaani kung’aa kwa nchi. Mtaalamu mwingine aliyewazia uendajikazi wa kifaa na kubuni istilahi inayokubalika mpaka sasa ni Prof. Rocha Chimerah ambaye alibuni istilahi ‘tarakilishi’. Pengine Prof. Chimerah alifikiria kazi ni kifaa husika na kuunda neno la Kiswahili linaloakisi kazi hiyo. Tunajua kwamba kompyuta hufanya kazi inayohusu tarakimu kwa haraka kama umeme. Labda Chimerah ameegemea sifa hii kuibuka na istilahi hii.
    Maneno mengine ambayo yamebuniwa kufuatana na msingi huu ni ya Mzee Nabhany-mathalan ‘barua pepe’ (e-mail), na wavuti (website). Tukiegemea maumbile, neno ‘kifaru’ lina maana ya vita ilihali tuna zana ya vita iliyopewa jina hilo kwa sababu ya labda kuwa na maumbile sawa na kifarumnyama. Nne, istilahi zinaweza kukopwa kutoka lugha nyingine. Yamkini hakuna lugha hata moja ulimwenguni-zikiwemo lugha duniani kama vile kiingereza zinazoweza kujitosheleza. Takriban asilimia 80 ya maneno katika kiingereza ni ya kukopwa. Kwa hivyo, lugha ya Kiswahili inapokopa, hali hiyo haipaswi kuchukuliwa kuwa ni lugha dhaifu.
    Hata hivyo, istilahi zinazokopwa zi-nafaa zichukuliwe zilivyo katika umbo lao asili. Umbo hili linaweza kufanyiwa marekebisho machache tu, kulingana na sarufi na matumizi ya lugha kopaji. Mifano ya istilahi kama hizi ni ‘televisheni’ (television), kopmpyuta (computer), kioski (kutokana na jina ‘kiosk’ la Kijerumani) na redio (radio), Tano, pale istilahi haiwezi kukopwa, lugha husika ijaribu kubuni msamiati ufaao, kufanya hivyo ni kuhakikisha kwamba, lugha inastawi. Lakini tahadhari inapaswa kuchukuliwa hivi kwamba, Kiswahili kisikope maneno kiasi cha kupoteza upekee wake. Mwisho, uundaji wa istilahi uzingatie mofolojia ya kawaida ya lugha. Istilahi zinazoundwa kwa kuzingatia mofolojia huwa rahisi kuiua maneno yenye uhusiano wa istilahi asili kwa njia ya mnyambuliko.



    (i) Taja mambo ambayo huchangia ukuaji na ufanisi wa jumla wa lugha ya Kiswahili
    (ii) “Lugha ya Kiswahili ni dhaifu na isiyotosheleza” Je, mwandishi wa makala haya
    ana msimamo upi kuhusu kauli hii?
    (iii) Tahadhari zipi zinazofaa kuchukuliwa kabla ya kukopa istilahi kutoka lugha zingine?
    (iv) Yape makala haya anwani mwafaka
    (v) Eleza maana ya maneno yafuatayo:
    (a) Dhana-
    (b) Takribani –
    (c) Istilahi – .
    (d) Mofolojia –...

    Date posted: October 4, 2019 .    Answers (1)