Get premium membership and access revision papers, questions with answers as well as video lessons.

Bondo District-Kiswahili Paper 2 Question Paper

Bondo District-Kiswahili Paper 2 

Course:Secondary Level

Institution: Kcse question papers

Exam Year:2006



102/2
LUGHA
1. UFAHAMU
Soma kifungu kifuatacho kisha ujibu maswali
Tangu zama kongwe za mawe maisha ya binadamu yamepitia katika awamu mbalimbali za kimaendeleo; yawe ya kisayansi, kiuchumi, kijamii au hata kisiasa. Katika kipindi chote ambacho binadamu ameishi katika ulimwengu huu, utamaduni umekuwa sehemu muhimu ya maisha yake. Utamaduni huu unaweza kuangaliwa kwa namna mbalimbali. Upo utamaduni finyu ambao unahusisha jamii moja dogo mathalan, kabila, ukoo au eneo dogo. Kwa upande mwingine kuna utamaduni pana ambao unaihusisha jamii nzima. Mathalan, nchi fulani inaweza kuwa na matendo, imani, thamani na fikira ambazo ni msingi mkubwa katika nchi hiyo. Hizi huwa msingi wa utamaduni wa kitaifa. Utamaduni huu ndio ambao unamtenga raia wa nchi moja na raia wa nchi nyingine. Utamaduni wa kitaifa ni nguzo muhimu ya uzalendo wa wanataifa maalum; unawatambulisha na wanauonea fahari. Vipengele vya utamaduni wa kitaifa huweza kutokeza kwa njia mbalimbali kama mavazi, vyakula, lugha, itikadi au hata mtazamo wa raia wa nchi mahsusi. Tumbi kubwa ya nchi za ulimwengu huwa na utamaduni unaozitambulisha na ambao humfanya raia ajinabi kuweza kuwatambua raia hao. Utamaduni ni kitovu cha uhai wa jamii yoyote ile. Licha ya ukweli huu, ni muhimu, inahalisi kutambua kuwa maisha ya binadamu huathiriwa na kani mbalimbali zinazotokea katika mazingira yake ya kila siku. Kani hizi huweza kuwa vyanzo vya mabadiliko ya sifa fulani zinazohusishwa na utamaduni wake. Maendeleo ya kiwakati ambayo huenda sambamba na mahitaji anuwai ya kimaisha huweza kuwa chanzo cha kuachwa kwa tamaduni fulani. Hata hivyo, binadamu sio sifongo ambalo hufyonza maji yote, maji machafu na maji safi pasi na kubagua. Binadamu mwenye akili razini anapaswa kuchuja na kutathmini ni amali au thamani zipi mpya ambazo anaweza kuzichukua na labda kupuuza baadhi ya thamani za kale zisizomfaa. Kigezo kikuu kinachomsaidia ni kutambua mahitaji yake sambamba na wakati anamoishi. Mathalan, katika maisha ya zamani, uchumaji ulitegemea ubabe kwa kiasi kikubwa lakini siku hizi ubabe sio kigezo cha uchumaji kwa kiasi kikubwa. Akili ni msingi mkubwa sana siku hizi katika uchumaji au kutarazaki. Inahalisi basi kupuuza sifa za kitamaduni ambazo zinaelekea kuutilia mkazo mkubwa kwenye matumizi ya nguvu au ubabe. Yapo matendo mengi katika jamii ambayo yalidhibitiwa na imani za kishirikina kabla ya nuru ya elimu kulimulika giza la ujinga lilitotamalaki katika jamii. Ikiwa jamii itaendelea kuyatenda matendo hayo basi ile itakuwa ni jamii ambayo, kama pia, imezunguka palepale. Ile itakuwa ni jamii ambayo imeshindwa kuendelea.
MASWALI
a) Taarifa hii inahusisha utamaduni na wakati kwa jinsi gani? (Alama 2) *BND*
b) Eleza uwili unaojitokeza katika utamaduni (alama 2) *BND*
c) Eleza dhima ya utamaduni ukirejelea taarifa (Alama 3) *BND*
d) Taja methali moja ukieleza matumizi yake inayofumbata ujumbe ulioko katika
taarifa hii (Alama 2) *BND*
e) Eleza mambo yanayopewa kipau mbele katika mchujo wa utamaduni (alama 2) *BND*
f) Uchumaji katika jamii umeathiriwa na wakati. Tathmini (alama 2) *BND*
g) Eleza maana ya vifungu vifuatavyo kama vilivyotumika katika taarifa husika.(alama 2)
*BND*
(i) Raia ajinabi
(ii) Giza la ujinga lililotamalaki

2. UFUPISHO
Soma kisha ujibu maswali
Vijana wanapaswa waelewe umuhimu wa kurekebisha tabia. Hakuna haja ya kijana kufura kama kaimati anapoaswa. Mtu akikukanya jambo usichukulie kuwa hakupendi na wala usimfanyie kiburi kwani kufanya hivyo ni kinyume cha uungwana na utamkatisha tamaa mwenye kukurudi na akikuacha bila kukuonya utapata hasara na kukiona cha mtema kuni.

Ni lazima wazazi wawaeleze watoto wao vile ambavyo walirekebishwa tabia zao zamani. Ifahamike kuwa wazazi walipewa adhabu kali kuliko hata zile wanazowapa watoto wao wa leo. Jambo la kushangaza ni kuwa ingawa waliadhibiwa hawakuwanunia wazazi wao bali waliwashukuru. Wazazi wengi wanadhani kuwa kufaulu kwao katika maisha kunahusiana sana na vile walivyofunzwa tabia nzuri. Wengi wanatoa shukrani kwa kuwatunza wakiwa hata wakongwe. Wanawapa heshima maalum ambayo si ajabu itakuwa nadra sana kupewa wakongwe wa miaka ijayo.

Binadamu gani anayekuwa bila kuonywa na bado awe mtu wa kuthaminiwa? Kama hata yai huguswa, sembuse wewe mtoto wa binadamu? Kwa nini usiguswe? Lazima uonywe hapa na pale, uadhibiwe inapopasa, ufokewe ukikosa au hata ukizidi uchapwe. Watu wote wanaohusika hasa wazazi na walimu yapasa wakuase wewe mtoto vilivyo mara unapotoka bila kukudekeza. Pia unatakiwa uombe msamaha unapokosa na kuahidi kutofanya makosa tena.

Kijana asipoangaliwa ataweza kuzuzuliwa na ujana ambao mwenyewe hajui kuwa ni kama maua, huja na kwenda. Ujana pia ni kama tembo la mnazi, huvuruga watu akili wakawa waongo, wenye dharau, wenye midomo michafu na nduma kuwili ambayo huleta zogo na zahama. Wengi huwa ni vitisho visivyo na mbele wala nyuma na wengine hawapendi kutumwa jambo kwa ugoigoi walio nao.

Badala ya kuwa washika adabu na washika dini, kuwa na bidii na wenye nyama ya ulimi, wao hukosa utu na huharibu wakati wao kwa kutakiana matanga badala ya kuombeana heri. Vijana kama hao huwadharau wenzao wanaojitahidi kuwa wazuri na kusema ni mazumbukuku waliozubaa sana. Pia husema wenzao wanajigamba kwa wazazi na walimu ili wapendwe. Yote hayo ni kijicho, wanawaonea wivu kwa uzuri wao.

Vijana wanaodharauliwa namna hiyo na kusemekana kuwa ni mbumbumbu mzungu wa reli kwa kuzuiliwa tu wasikate tamaa. Watie bidii kila mahali, wafaulu. Hao ndio watakaopata radhi za wazazi wao. Kwanza hufanikiwa sana maishani, huwa waadilifu na viongozi bora wa baadaye. Kule kusema sana kwa kuwa maarufu katika mambo ya kijinga sio kuendelea ni kujipoteza. Watoto wazuri hawazozani, huepuka tandabelua za aina yoyote, hutulia kama maji mtungini. Yafaa ikumbukwe kuwa anayejitenga na maovu haingii hatiani. Waswahili hawakukosea waliposema kuwa aliye kando haangukiwi na mti.

Inatakiwa kijana ajiase na kujiuliza wapi ujana huo unamwelekeza na ukimtoka atakuwa ni mtu wa namna gani. Pia ajiulize kuwa uzee utamkuta akiwa amejijenga kitabia na kiuchumi ama atabaki akipiga malapa na kuwa kupe mjini. Ni vizuri pia ajue uhusiano wake na wazazi wake ulivyo na kuhakikisha kuwa ametenda ya kumfanya apate dhima ama ya kumfanya asionekane kama kibaparu tu.

Ingawa leo watu wanazidi kuamini kuwa mtoto umleavyo ndivyo akuavyo, sikubaliani na msemo huo mara nyingi. Wakati mwingine si kweli. Kuna wakati inapofaa hata kusema mtoto umleavyo sivyo akuavyo. Labda umewahi kuona hapa na pale visa vya watoto waliolelewa wakaleleka, watoto wa viongozi wa dini na watoto wa wazazi wa kuheshimiwa ambao wameharibika. Labda wemekuwa hivyo kwa sababu ya umri, mazingira na kuchanganyika na marafiki wabaya. Watoto hao huzuzuka ghafla na kwa siri bila ya wazazi kujua na hata wakija kushtukia wanagundua kuwa watoto wameota sugu. Wazazi wanaweza kulea vizuri lakini matokeo ya malezi mara nyingi ni kama majaliwa tu. Watoto wote wanaweza kuwa wazuri lakini pakatokea mmoja kati yao wa kuleta kisirani akawa shetani kupindukia.

Wazazi huchukua hatua ya kuwakanya watoto wabaya lakini wengine hawasemeki. Mara nyingine huwapeleka hospitali wakiwadhani ni wagonjwa wa akili, ama, kutafuta marafiki wa kuwazungumzia lakini yote hayo hayafui dafu. Watoto hao watakuwa kama kitu cha kuvunda na hata uweke manukato gani uvundo hautaisha bali utahimikiza kila mahali. Wewe kama mzazi utaazirika lakini wao watajitia hamnazo na kukaza kamba na kufanya wayapendayo. Kwanza kama hao hawatambui juhudi za wazazi na badala yake wanawaona wazazi kama mashua ivushayo lakini mbovu.

Wewe kama mzazi ukipatwa na balaa kama hiyo utasemaje? Umeambulia patupu. Ungeleaje? Bila shaka utatindikwa na maarifa na labda utaamua umwache mtoto huyo kufunzwa na ulimwengu. Jambo utakalo jifariji nalo ni kuwa hukumkosea huyo mtoto, umetimiza wajibu wako kama mzazi kwa kumkimu kwa kila hali, kumfunza elimu na dini ya kidunia na kwa kumpeleka shule ingawa kwa maajabu ya Firauni yamekupata hayo makubwa. Labda utabaki ukimuomba Mola muweza akakutengenezee ili mtoto apate kubadilika

Kutumia mabavu katika kumrekebisha tabia ni kuzidi kumharibu kwani ni kama kumkunja samaki mkavu au kutarajia mazingaombwe. Mtoto amelilia wembe, umemkanya hasikii basi utampa. Hakuna haja ya kuubanzabanza, wembe huo unaweza kukukata. Kweli uchungu wa mwana unao, lakini kung’ang’ania hivyo na mambo kama haya ni kijiumiza na kujiletea vidonda tumboni na kupata mvi za mapema mapema. Utakuwa unapiga ngumi ukutani. Katika hali kama hii wazazi wengine huamua kushika hamsini zao na kushughulikia mambo menginie yaliyo na maana zaidi.

Kijana kama huyo akiona umemwingilia sana atagura aende kutafuta atakachokiita amani na furaha. Atauingilia ulimwengu kikuku. Huenda akataka kuishi mjini ambako atalifanya atakalo bila ushauri wa mtu yeyote, kwa kuwa kila mkuu wake ni tambara mbovu.

Mambo yanaweza kumwendea vizuri mwanzoni. Huenda akapata marafiki wa uongo na mashabiki vichwa maji kumshinda yeye hata mara kumi kwa ujuba wa kimji. Huenda kijana huyo akaona amefika kilele cha ufanisi na aishi maisha ya ufahari. Huenda akabadilisha marafiki na magari kama nguo. Huenda akasema anapendwa kupindukia na kuona kuwa wale wazimbukuku wa nyumbani watamchoka. Hayo yote si kitu, mji utakuja kumtoa ushamba.

Inawezekana siku moja kijana huyo asingiziwe jambo kubwa la kumfanya atiwe ndani baada ya urafiki wao wa kula na vivuli unapomalizika. Hapo labda atakimbiwa na marafikize na kujiingiza katika kisima alichojichimbia mwenyewe. Atagundua kuwa ulimwengu umemfunza . Wazazi pamoja na ndugu watakapopata habari zake watafunga safari mara moja kwenda kumwepua au kumwona. Watafanya hivyo si kwa kuwa walimtuma akatende maovu, ila kwa kuwa damu ni nzito kuliko maji. Mtoto akiwaona hao wazazi na ndugu zake waliokuja kumwauni ataaibika na kujua kuwa kwa kweli mla nawe hafi nawe ila mzaliwa nawe.

MASWALI
a) Fupisha aya saba za mwanzo kwa maneno 90 – 100 (alama 7) *BND*
b) Mtoto umleavyo sivyo akuavyo. Eleza kwa maneno kati ya 60 – 70 (alama 8) *BND*
3. MATUMIZI YA LUGHA
a) Majina haya hupatikana katika ngeli gani (alama 4) *BND*
(i) Sukari .................................................................................................................................................
(ii) Kiongozi ............................................................................................................................................
(iii) Gari.....................................................................................................................................................
(iv) Kalamu ................................................................................................................................................
b) Andika sentensi moja yenye viungo vifuatavyo (alama 3) *BND*
(i) Kikanushi
(ii) Kiima katika nafsi ya pili wingi
(iii) Mtendewa katika nafsi ya tatu umoja
(iv) Wakati uliopita
(v) Kauli ya kutendea
(vi) Shina / Mzizi wa kitenzi
c) Tunga sentensi ukitumia neno ’haya’ kama (alama 3) *BND*
(i) Kiwakilishi
(ii) Jina
(iii) Kivumishi
d) Ainisha vielezi katika sentensi ifuatayo. (alama 3) *BND*
Mwanafunzi mzuri ni yule afanyaye mazoezi vizuri kila siku shuleni

e) Andika sentensi ifuatayo katika usemi halisi
Wakili alimtahadharisha mshukiwa kwamba asingemwarifu ukweli wote kuhusu kesi hiyo asingemwakilisha (alama 2) *BND*
f) Andika sentensi ifuatayo katika ukubwa na udogo
Mbuzi yuyu huyu alikula mimea ya mwanamke yule (alama 2) *BND*
g) Tumia ‘o’ rejeshi ya mazoea katika sentensi ifuatayo.
Mti ambao ulikatwa ulipelekwa kiwandani (alama 1) *BND*
h) Onyesha kundi nomino na kundi tenzi katika sentensi ifuatayo
Mwanafunzi wetu mwerevu alitembea haraka lakini hakufika mapema (alama 2) *BND*
i) Ainisha nomino katika sentensi ifuatayo .
Kucheza kwa Juma kulikipa furaha kikosi cha askari (alama 4) *BND*
j) Geuza kitenzi kiwe jina ukikanusha
Juma ameoa mwanamke mrembo mithili ya hurulaini (alama 1) *BND*
k) Tunga sentensi moja ukitumia kitenzi halisi na kitenzi kisaidizi (alama 1) *BND*
l) Eleza jinsi neno ‘kwetu’ lilivyotumika katika sentensin zifuatazo (alama 3) *BND*
(i) Juma ameenda kwetu.
(ii) Kwetu ni kule
(iii) Mahali kwetu ni kule
m) Tunga sentensi moja ukionyesha shamirisho kipozi na shamirisho kitondo.(alama 2) *BND*
n) Eleza maana na matumizi ya methali ifuatayo
Angaruka juu kipungu hafikilii mbinguni (alama 2) *BND*
o) Andika visawe mwafaka (alama 2) *BND*
(i) Hau…………………………………………………………………………………………………
(ii) Bohari…............................................................................................................................................
p) Tunga sentensi ukitumia semi zifuatazo (alama 2) *BND*
(i) Piga bweu.............................................................................................................................
(ii)Kazi ya papara papara………………………………………………………………………
q) Tumia neno hili kutunga sentensi tatu zenye maana tofauti
Kina (alama 3) *BND*
4 ISIMU JAMII
a) Eleza maana ya Isimu jamii (alama 1) *BND*
b) Eleza maana ya dhana zifuatazo za simu ya jamii (alama 3) *BND*
(i) Msimbo
(ii) Lafudhi.
(iii) Lahaja.
c) MTU (i): Hamjambo mabwana na bibi?
WOTE (ii): Hatujambo.
MTU (i): Ahsante sana.
MTU (iii): Bwana mwenyekiti, huyu alituma maombi kutaka kuajiriwa kama naibu wa msajili
katika idara ya usajili chuoni
MTU (ii) Wewe ndiye Kazikwisha Mzaliwa?
(i) Tambua wazungumzaji wote watatu katika mazungumzo haya (alama 1 ½) *BND*
(ii) Hii ni sajili ipi ya lugha? (alama ½) *BND*
(iii) Eleza sifa zozote nne za sajili hii ya lugha ukirejelea kifungu ulichopewa. (alama 4) *BND*











More Question Papers


Popular Exams



Return to Question Papers